Saturday, March 8, 2014

TFF YAWAPA WAKATI MGUMU YANGA

UONGOZI wa Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF) umeonyesha uzembe wa wazi kutokana
na aliyetakiwa kuwa mkuu wa msafara wa
Yanga iliyo mjini hapa anayetokea katika
shirikisho hilo , kutokuwa amewasili jijini hapa
hadi jana mchana.
Ilielezwa mjumbe aliyeteuliwa na TFF kuwa
kiongozi wa msafara alikuwa hajawasili na
kuifanya Yanga kuwa na wakati mgumu wa
mawasiliano.
Kwa kawaida , mwakilishi wa TFF ambaye ni
kiongozi wa msafara wa Yanga, alitakiwa
kufanya mawasiliano yote na Shirikisho la Soka
Afrika (Caf ) na lile la Misri (Efa ), lakini
hakuwepo.
Akizungumza, Makamu Mwenyekiti wa Yanga ,
Clement Sanga, alithibitisha kwamba kweli
kiongozi huyo wa msafara hakuwa amefika na
kazi zake nyingi zimekuwa zikifanywa na
maofisa wa ubalozi .
“Kweli hajafika na ninaweza kusema tunapata
ugumu wa mawasiliano maana Caf na
shirikisho lao linataka mtu kutoka kwenye
shirikisho letu . Sasa hayupo na ndiyo
tunaendelea kupambana tu,” alisema Sanga.
Kawaida kiongozi wa msafara hutakiwa
kuongozana na timu mwanzo hadi mwisho wa
mapambano.
Kama huyo wa TFF atakuwa amewasili leo ,
basi atakuwa amekuja Misri kuangalia mechi
kama watazamaji wengine .

No comments:

Post a Comment